Home Back

Kariakoo ngoma mbichi

mwananchi.co.tz 2024/7/7

Dar es Salaam. Licha ya Serikali kutangaza kuwa itafanyia kazi malalamiko ya wafanyabiashara wa Kariakoo, ikiwemo kusitisha kamatakamata iliyokuwa ikifanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), baadhi ya wafanyabiashara wamesema Rais Samia Suluhu Hassan ndiye anapaswa kutoa tangazo hilo.. 

Wamesema kauli ya Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo haiwezi kuwafanya wafungue maduka,  huku wakidai kuwa matamko ya viongozi wengi huwa yanapuuzwa na taasisi za Serikali, hivyo labda mkuu wa nchi akizungumza watamasikiliza.

Wafanyabiashara hao walitoa kauli hiyo jana walipozungumza na Mwananchi, ikiwa ni  muda mfupi kupita tangu Serikali kupitia Profesa Mkumbo,  kutoa msimamo wake juu ya mgomo uliokuwa ukiendelea katika eneo la  Kariakoo jijini Dar es Salaam tangu jana asubuhi.

Mgomo huo ulioitishwa na wafanyabiashara, unalenga kuishinikiza Serikali kusikiliza malalamiko yao ya utitiri wa kodi wanazolipishwa na TRA na kamatakamata ya mizigo yao, huku wakidai wachuuzi hawatoi risiti za kielektroniki.

Baada ya saa zaidi ya tisa za mgomo huo jana, hatimaye saa 10 jioni Serikali kupitia Profesa Mkumbo, ilitangaza maazimio sita yaliyofikiwa katika kikao cha mawaziri na viongozi wa wafanyabiashara hao kilichofanyika jijini  Dodoma.

Profesa Mkumbo alisema Serikali imesitisha kazi ya ukaguzi wa risiti za kielektroniki (EFD) na ritani za kodi, kazi iliyokuwa ikifanywa na TRA kupitia mkoa wa kikodi wa Karikaoo,  huku ikiandaa utaratibu mzuri wa utekelezaji wa suala hilo.

“Pia tumekubaliana kuwapanga machinga ili kutoingilia ufanyaji biashara wa wenye maduka na kuhakikisha kila anayefanya biashara analipa kodi kama ilivyokubalika,” alisema Profesa Mkumbo.

Kuhusu changamoto zilizoibuliwa na kamati ya wafanyabiashara iliyoundwa baada ya mgomo wa mwaka jana, Profesa Mkumbo alisema iliibua changamoto 41 na 35 zinahusu utendaji na sita zinahusu sheria ambazo bado zinafanyiwa kazi.

Wazungumzia kauli ya waziri

Wakizungumzia kauli ya Waziri Mkumbo, mfanyabiashara Vennance Sanga, alisema kuna matamko yanayotolewa ambayo hayawasaidii wafanyabiashara.

Alisema mengi ni kama zimamoto yenye lengo la kuwapoza pale wanapopaza sauti zao.

"Walishatoa matamko mwaka jana hadi kufikia hatua Waziri Mkuu kuingilia kati, lakini hayafanyiwi kazi, kuzungumzia masuala ya risiti sio tatizo tunalolalamikia peke yake, yapo mengi pamoja na wateja wetu kuchukuliwa na wageni,” alisema Sanga.

Alisema kumeibuka tabia ya watu waliofika nchini kama wawekezaji kuuziana mizigo na wateja wao wanatoka nje ya nchi kwa kuwaambia watawaletea mizigo kwa bei ya kiwandani.

Sanga alisema hata walipopeleka malalamiko hayo kwa wahusika, hawakupatiwa majibu na matokeo yake kuona kama kuna mchezo unafanyika baina yao.

"Haiwezekani wawekezaji waongee biashara na wateja wetu ambao wanatoka nje ya nchi wakija hapa wanakutana na hao watu sisi tunapata nini hapo zaidi ya kubaki na mizigo yetu kwa sababu watafuata unafuu huko," alisema.

Alisema kauli hiyo ya Waziri haiwezi kuwashawishi kufungua maduka yao na ikiwezekana kauli itoke kwa Rais Samia,  huku akidai wanahisi kuna watu wanaomhujumu.

Mfanyabiashara wa duka la simu, Ashura Mohamed alisema wanacholilia ni kamatakamata na si suala la ukaguzi wa risiti kwa sababu kilio chao ni cha mizigo yao na wateja kukamatwa bila maelezo.

"Wanatutolea matamko wakati tunataka vitendo ni ngumu kufanyia kazi hayo mtu anakamatwa akiwa amenunua mzigo wa Sh800,000 anaambiwa alipe faini Sh2 milioni anaona bora auache tu," alisema Ashura.

Muuza nguo, Ashraf Mwinyi alisema tabia ya kuwatuliza kwa matamko kwa sasa hayana nafasi zaidi ya kuendelea na msimamo wao ili Serikali ijue kuwa wafanyabiashara wanaumia na yanayoendelea.

"Tunatuma wawakilishi lakini kinachotokea wanatunga sheria ambazo zinatuumiza bila kujali maslahi ya wananchi. Leo hii wanakuja na kauli nyepesi ya kuondoa ukaguzi wakati kuna mambo mengi tumeyalalamikia hayajafanyiwa kazi," alisema.

Walimuomba Rais aingilie kati kilio chao kwani wanateseka na nchi inapoteza mapato kwa ajili ya watu wachache wanaojali maslahi yao binafsi

Hali ilivyokuwa

Tangu Mwananchi inafika sokoni hapo mapema asubuhi jana, machinga pekee ndiyo walikuwa wakitoa huduma ya kuuza bidhaa mbalimbali.

Kelele zao za kutangaza bei ndiyo pekee zilizosikika zikiita wateja huku na kule, wengine wakiwaambia wateja kuwa wao ndiyo wanaweza kuwahudumia na hakuna duka lililokuwa wazi.

Hali hiyo iliibua usumbufu kwa wachuuzi wa bidhaa mbalimbali katika soko hilo,  wakiwamo wanaotoka mikoani na nchi jirani baada ya kushindwa kujua hatma yao.

Hiyo ni baada ya kukuta maduka yamefungwa kufuatia mgomo ulioitishwa na uliosababisha washindwe kununua bidhaa,  huku baadhi waliokuwa wamenunua mzigo kabla ya mgomo wakihangaika kutafuta wamiliki wa maduka wafungue ili wachukue mizigo yao.

“Unajua kabla sijatoka jana nyumbani (Mbeya) kuja huku niliona hicho kipeperushi nikajaribu kuuliza kuhusu huo mgomo baadhi wakaniambia haujatangazwa na mwenyekiti, basi wakanipa moyo kuwa hautakuwepo matokeo yake nimekwama,” alisema Silvester Mwaipopo ambaye ni mfanyabiashara.

Alisema lengo lake lilikuwa kuondoka na gari la usiku jana kurudi jijini Mbeya,  lakini ratiba yake haikwenda vile alivyopanga.

“Sikujua kama kuna mgomo, nia yangu ni kufunga mzigo leo na nilipofika hapa nimekuta maduka yote yamefungwa. Nilipouliza nikaambiwa leo hatufungui, nilitarajia kuondoka kesho (leo) sasa naona gharama itaongezeka,” alisema Grace mfanyabiashara kutoka Zambia

Mfanyabiashara mwingine kutoka Zambia, Sophia Banda alisema mgomo unaoendelea unafukuza wateja na kutokuwepo kwa soko la uhakika,  hivyo Serikali inatakiwa kukaa na wafanyabiashara kusikiliza malalamiko yao.

"Tunafuata mizigo Tanzania kwa sababu ya uhakika wa soko, sasa kama kunakuwa na migomo ya ghafla bila kupatiwa taarifa,  wateja itatubidi kutafuta soko nchi nyingine kwani inatuongezea gharama ya kuishi hapa nchini," alisema Banda.

 Licha ya kuwa maduka hayakufunguliwa, wafanyabiashara walifika katika maduka yao mapema kama ilivyo kawaida yao lakini walikaa nje na kupiga stori.

Wote walikuwa wakisubiri kupatiwa majibu yanayoeleweka kabla ya kuendelea na shughuli zao hasa juu ya kero walizokuwa wanazilalamikia.

Mfanyabiashara Martha Masanja alisema tangu alipofika saa moja asubuhi alishindwa kufungua duka lake baada ya kukuta wenzake wote wamefunga.

“Kero kubwa ni TRA mimi niko hapa kusaidia sauti isikike, hatujajua watatuambia tufungue saa ngapi ila tunasubiri,” alisema Martha.

 “Viongozi hawapo upande wetu, tangu mwaka jana tulipogoma malalamiko yetu hayajapewa majibu, tungekuwa tumepewa tusingegoma, ile tume iliyoundwa haikuja na majibu ya yale yaliyofikiwa,” alisema mfanyabiashara Lazaro Michael.

Machinga kicheko

Wakati sehemu ya uhakika ya kupata bidhaa kwa wateja kwa jana ikiwa ni kwa machinga, wenyewe waliuita mgomo huo kama siku ya neema huku wakiufananisha na methali isemayo hasira za mkizi furaha kwa mvuvi.

“Leo ni kama sikukuu, wateja wote kwetu, vita ipo kati yetu wenyewe siyo na wenye maduka, alisema Richard Steven ambaye alikuwa akiuza nguo za kiume.

Hata hivyo, kutofunguliwa kwa maduka kulifanya baadhi ya bidhaa zinazouzwa na machinga sokoni hapo kupanda bei jambo ambalo lilifanya wanunuzi walipie zaidi.

Akitolea mfano wa viatu ambavyo vilinunuliwa kwa Sh8,000 kabla ya mgomo  viliuzwa kwa Sh9,000 hadi Sh10,000 bila ya kuwapo kwa punguzo.

Chalamila agonga mwamba

Baada ya kuwapo kwa kelele nyingi katika mitandao ya kijamii, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila alifika sokoni hapo akiongozana na viongozi wengine akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo.

Chalamila aliweka bayana msimamo wake wa kuendelea kuwalinda watakaokuwa tayari kufungua maduka yao.

Akiwa eneo hilo, aliwasihi wamachinga kuendelea na shughuli zao huku akizungumzia namna wamiliki wa maduka wanavyolalamikia uwepo wao na kutaka waondoke ila msimamo wake ni kutowaondoa.

Chalamila pia alizungumzia juu ya malalamiko ya uwepo wa wafanyabiashara kutoka China wanaofanya shughuli ndogondogo ambao wamekuwa wakilalamikiwa na wafanyabiashara.

Hali hiyo iliwafanya baadhi ya wafanyabiashara kuonyesha kutoridhishwa na kile alichokisema mkuu wa mkoa huku akiwataka warejee katika shughuli zao.

“Mkuu wewe umekuja huku kuongea na wafanyabiashara siyo machinga. Machinga hawajagoma wanaendelea na shughuli zao sisi ndiyo tumegoma,” alipaza sauti mmoja wa wafanyabiashara akiwa juu ya ghorofa.

Wakati huyo akiibuka na hoja hiyo alitokea mwingine na kusema wamachinga hawalipi kodi hivyo si rahisi kugoma.

Chalamila alimjibu kuwa wamachinga nao ni wafanyabiashara wakubwa wa kesho.

Alisema kitu anachopenda ni mazungumzo lakini pindi anapotishiwa na kushinikizwa huwa hafanyi kile kinachohitajika.

“Huwa natamani tukae mezani tuelewane, ukiigeuza biashara kuwa siasa siwezi kukusikiliza.Mimi siyo kiongozi wa chama cha siasa, mimi nalea wafanyabiashara wote bila kujali wanatoka wapi wanakwenda wapi,” alisema Chalamila na kuongeza:

“Migomo siyo suluhisho bali kukaa mezani na kuzungumza ndiyo jambo linaloweza kujenga Dar es Salaam.”

Kuhusu kodi alisema kiwango cha ukwepaji bado kikubwa huku akieleza kuwa baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakitishia kugoma pindi TRA inapojaribu kufuatilia utoaji wa risiti.

Alisema kabla ya kuwapo kwa biashara, sheria zilikuwepo hivyo kama mtu alizisoma na kuzielewa, inakuwaje  watu wanalia huku akisema kama watu waliona sheria si rafiki wangekataa.

“Sasa kuanza kunishinikiza leoleo, nibadilishe dunia leoleo haiwezekani, Sasa mimi nimeahidi kulinda biashara zote, ikiwezekana baadaye kama itahitajika kuweka vyombo vya dola nitaweka ili kote kufungwe halafu tusubiri hadi tusuluhishe. Kama itachukua miezi miwili sisi tutalinda kwa miezi miwili hakuna mtu atainama kufungua kufuli,” alisema Chalamila. 

Alisema Serikali haishindwi jambo, kama  imetuma vikosi Congo na Sudan (Darfur) kwenda kupigana haiwezi kushindwa kwenda Kariakoo.

“Hapa cha kujiuliza itakuwa ni biashara? kama unapata Sh200 leo faida Sh100 basi endelea mazingira yakiwa mazuri kesho utapata Sh400, sasa ukifunga unapata nini,” alihoji Chalamila.

Hata hivyo, wakati maduka mengine yakiwa yamefungwa, wauzaji wa dawa za asili waliendelea na biashara kwa madai kuwa wao wanatoa huduma za hospitali kunusuru uhai wa binadamu.

"Sisi ni kama madaktari hivyo tunatoa huduma lakini tupo pamoja na wenzetu kwa sababu madai yanayotolewa hata sisi yanatugusa kwenye suala la kodi," alisema Asma Mcheche.

People are also reading